Ulaya bado inaonekana kufikiria kuhusu wazo kwamba vita kwa mara nyingine tena vimelikumba bara hilo baada ya miongo kadhaa ya amani.
Uvamizi wa Urusi katika rasi ya Crimea ya Ukraine mwaka 2014 ulitoa tahadhari kote Ulaya.
Hili lilikuwa onyo la kwanza. La pili lilikuja Februari 24, 2022, wakati serikali ya Vladimir Putin ilipoanzisha uvamizi wa kijeshi wa kushangaza, umwagaji damu, na uvamizi kamili wa kijeshi dhidi ya Ukraine.
Takwimu zinaonyesha kuwa Ulaya ina wasiwasi juu ya usalama wake na inakabiliwa na changamoto tatu: kuendelea kuandaa jeshi la Volodymyr Zelensky, kuboresha silaha zake, kuajiri na kutoa mafunzo ya askari wake, au hata kurudi kweneye mfumo wa zamani wa huduma ya lazima ya kijeshi.
Katika muktadha huu mpya, wanachama wengi wa Ulaya wa Shirika la kujihami la nchi za Magharibi (NATO) waliongeza matumizi yao ya kijeshi mwaka jana. Sehemu yao ya pamoja iliwakilisha 28% ya bajeti ya jumla ya muungano huo, ikiwa ni bajeti ya juu zaidi kutumika katika muongo mmoja, kulingana na utafiti uliofanywa na Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Amani ya Stockholm (SIPRI).
"Tangu 2014, NATO imepitia mabadiliko makubwa zaidi ya ulinzi wa pamoja kuwahi kushuhudiwa katika kizazi. Tumeweka mipango kamili ya ulinzi tangu Vita Baridi, na zaidi ya wanajeshi 500,000 wako tayari leo," ofisi ya mawasiliano ya shirika hilo lenye makao yake mjini Brussels iliiambia BBC Mundo.
Nchi zinazounda muungano huu wa mashariki, ambao pia unafahamika kama "Bucharest tisa", ni zile za zilizopo kijiografia karibu na Urusi: Bulgaria, Jamhuri ya Czech, Estonia, Hungary, Latvia, Lithuania, Poland, Romania na Slovakia, pamoja na wageni Sweden na Finland.
Ukraine na Magharibi zina mawazo tofauti kuhusu kuishinda Urusi - Zelenskyi
Je, kutumia silaha za Magharibi dhidi ya Urusi kutasaidia Ukraine kuvibadili vita?
"Kwa nchi wanachama wa NATO, miaka miwili iliyopita ya vita nchini Ukraine imebadilisha mtazamo wa usalama," anasema Lorenzo Scarazzato, mtafiti katika mpango wa matumizi ya kijeshi na uzalishaji wa silaha wa SIPRI.
"Mabadiliko haya katika mtazamo wa tisho yanaonekana katika kuongezeka kwa idadi ya Pato la Taifa miongoni mwa wanachama linalotengwa kwa ajili ya matumizi ya kijeshi, na lengo la 2% la NATO linazidi kuonekana kama alama badala ya kizingiti cha kupatikana," anaongeza.
Matumizi ya silaha zinazojiongoza
Lakini wachambuzi wengi wanaonya kuwa haiwezekani kuongeza matumizi ya silaha bila kuathiri wafanyakazi.
Hii ndio sababu wazo la kurudi kwa usajili au aina fulani ya usajili imepata kasi katika miaka ya hivi karibuni katika nchi kadhaa za Ulaya.
"Jinsi tunavyowaajiri na kuwahifadhi wanajeshi ni uamuzi kwa washirika wetu. Karibu theluthi moja ya wanachama wa NATO wana aina fulani ya usajili na wengine wanaifikiria. Jambo muhimu ni kwamba washirika wanaendelea kuwa na vikosi vya kijeshi vyenye uwezo wa kulinda nchi zetu," msemaji wa NATO aliiambia BBC World.
Kulingana na masharti na viwango vya kujitolea, karibu nchi kumi za Ulaya hutumia aina fulani ya usajili au huduma ya kijeshi ya hiari: Sweden, Norway, Denmark, Finland, Austria, Estonia, Latvia, Lithuania, Ufaransa na Ugiriki.
Tofauti kati ya usajili wa wapiganaji na huduma ya kijeshi ya hiari ni kwamba katika siku za nyuma, wanaume wote (na wakati mwingine pia wanawake wote) wa umri fulani lazima wangetumikia nchi yao kwa kipindi fulani, lakini hawawezi kuitwa kwa huduma ya kazi.
Kwa mujibu wa wataalamu, hakuna nchi ya Ulaya inayoweza kukabiliana na mgogoro wa "kiwango cha juu" kama Ukraine na uwezo wake wa sasa.
Mabadiliko makubwa yalitokea katika nchi za Baltic na Scandinavia, kutokana na kuongezeka kwa mtazamo wa hatari ya uchokozi wa Urusi au kuongezeka kwa mgogoro.
"Nchi zote za Soviet ya zamani na Warsaw katika Ulaya ya Mashariki zimedumisha huduma ya lazima ya kijeshi. Moja ya sababu zilizo wazi ni hofu ya kurejea kwa Urusi katika eneo hilo na kuibuka tena kwa mtazamo wa kishujaa kwa upande wa jirani yake," Luis Velasco, profesa wa historia ya mahusiano ya kimataifa katika Chuo Kikuu cha Vigo ameiambia BBC Mundo.
"Lakini kwa nchi za Ulaya Magharibi, baada ya kuanguka kwa Ukuta wa Berlin, haikuwa na maana tena. Hakukuwa na sababu ya kudumisha idadi kubwa ya askari wa operesheni na askari wa akiba," anaongeza.
"Vuguvugu la amani, harakati za mazingira na hata harakati za wanawake pia zimeweka shinikizo kubwa la kijamii kukomesha usajili.
Ufahamu wa hatari
Latvia ni nchi ya hivi karibuni kuanzisha huduma ya lazima ya kijeshi. Ilianzisha tena huduma ya lazima ya kijeshi mnamo Januari 1 mwaka huu, baada ya kuifuta mnamo mwaka 2006. Lakini majirani zake wa Bahari ya Baltic pia wamechukua hatua haraka.
Lithuania iliachana na usajili mwaka 2008, lakini iliurejesha tena mwaka 2016 baada ya uvamizi wa kwanza wa Urusi nchini Ukraine mwaka 2014. Estonia imedumisha aina ya usajili wa kijeshi tangu ipate uhuru katika 1991.
Finland, ambayo hivi karibuni ilijiunga na NATO, imeendelea na huduma ya lazima ya kijeshi tangu Vita vya Pili vya Dunia na inakadiriwa kuvutia raia wa kiume 27,000 kujiunga na jeshi.
Majirani zake wawili wa Scandinavia sio tu wamerudi katika mfumo huu wa huduma ya lazima kwa jeshi , lakini pia wameanzisha usawa: wanawake lazima pia wafanye huduma ya kijeshi nchini Sweden na Norway.
Sweden, ambayo ilijiunga na NATO mwezi Machi, iliachana na usajili mwaka 2010 lakini ikaurejesha tena mwaka 2018 wakati nchi hiyo ikijiandaa kujiunga na NATO.
Mwezi Machi, Denmark ilitangaza mipango ya kuongeza huduma za lazima za kijeshi kwa wanawake kwa mara ya kwanza na kuongeza muda wa huduma kutoka miezi minne hadi 11.
"Baadhi ya nchi zina kiwango cha kipekee cha ufahamu wa ulinzi wa taifa, kama vile Finland, ambapo huduma za kijeshi zinakubaliwa vizuri na jamii, kwa karibu 90%," Francisco Gan Pampols, Luteni Jenerali mstaafu katika jeshi la Uhispania, aliiambia BBC Mundo.
Watu wa Norway wanaelewa vizuri sana tisho wanalokabiliana nalo na linatoka wapi, anaongeza.
Je, juhudi za vita zinaungwa mkono vipi?
"Na kuna nchi nyingine ambapo itakuwa vigumu kurejesha dhana hii kwa sababu hisia ya ulinzi wa kitaifa ni dhaifu sana. Ulinzi umeachwa kwa jeshi la kitaalamu ambalo linawajibika kwa hilo, "anaelezea Gan Pampols.
Lakini ukweli ni kwamba kwa sasa hakuna jeshi barani Ulaya ambalo linaweza kuendeleza juhudi za vita zinazohusika katika mgogoro kama Ukraine bila ya kuhamasisha rasilimali za ziada.
Wataalamu wanaeleza kuwa ni muhimu sio tu kuajiri askari zaidi, lakini pia kuwafundisha, kuwapeleka katika mstari wa mbele na kuwapa ruhusa wakati wa kurudi kwao. Na katika mzunguko huu, uingizwaji wa wanajeshi zaidi tayari unahitajika.
Changamoto nyingine ambayo nchi zinakabiliwa nayo ni kiwango cha teknolojia ya majeshi, ambayo imeongezeka kwa kiasi kikubwa.
"Utaalam unaongezeka, pale unapohitajika. Leo, nafasi katika jeshi ni nafasi ambazo zinahitaji mafunzo mengi na kisha mazoezi. Unahitaji kufanya mazoezi kwanza, kisha kufanya kazi. Na hiyo inachukua muda, "anaelezea Gan Pampols.
Anataja nafasi ya mwendeshaji wa droni kama mfano. Mafunzo ya majaribio ni mafupi, lakini lazima ufanye mazoezi ya kuiendesha usiku kwa kuielewa mifumo yake.
Hii ni michakato ambayo wakati unahitajika ili kuhakikisha mafanikio ya hali ya juu yanapatikana.
Utulivu wa kuepuka vita
"Hatujafanya hivyo kwa sababu tunataka vita. Tunakuwa na subira kwa sababu tunataka kuiepuka," Waziri Mkuu Mette Frederiksen alisema wakati akitangaza mipango ya kijeshi ya Denmark.
Huduma za ujasusi kijeshi zinakubaliana: lengo la mipango ya kuongeza bajeti ya Ulaya sio kupigana vita, lakini kumzuia adui, kuwa na mkakati wa kuaminika.
Na kwa hili, ni muhimu kuboresha silaha, lakini pia uwezo wa kibinadamu na mafunzo.
Serikali ya Olaf Scholz imezingatia kwamba wafanyakazi wa kijeshi wanaokabiliwa na kiwango cha hatari kinachowakabili sio sawa, na kwa hivyo inafikiria kuimarisha huduma ya lazima ya kijeshi.
Ujerumani ilipiga maruf*cku usajili mwaka 2011, lakini vita vya Urusi nchini Ukraine viliilazimisha kufikiria upya.
Kulinda mauzo ya nje
Kwa hatua hiyo, nchi itaonyesha kuwa ni ya kuaminika wakati wa kulinda mali yake ya thamani zaidi: mauzo yake ya nje. Ujerumani imeongeza bajeti yake ya ulinzi kwa sababu uwezo wake wa kiuchumi unategemea ukweli kwamba hakuna kitu kinachoweza kuhatarisha uzalishaji wake.
Ujerumani ilihesabu kuwa mgogoro wa kikanda utahatarisha mawasiliano yake, vifaa, na mauzo ya nje, na kwamba washirika wake wakuu barani Ulaya wataingia katika uchumi wa vita na kuacha kununua bidhaa zake.
Kuanzia mwaka 2022, Berlin imeahidi kuwekeza kwa kiasi kikubwa katika vikosi vyake, ambavyo inavichukulia kuwa vidogo na vilivyopitwa na wakati, ili kuwa na jukumu kubwa zaidi katika ulinzi wa Ulaya.
Lakini leo, kama ilivyo katika nchi nyingine zote za Ulaya Magharibi, serikali zimekuwa zikisita kuanzisha huduma ya lazima ya kijeshi.
"Sio tu kwamba haipendezwi na wale walioombwa kutumikia - na familia zao - lakini pia huondoa mtaji wa binadamu kutoka kwa wafanyikazi wa serikali na ina athari za kiuchumi," anaandika Rod Thornton, profesa wa masomo ya kimataifa, ulinzi na usalama katika King's College London, kwenye tovuti ya Mazungumzo.
Ramani ya kijiografia na kijeshi ya karibu nchi zote za Ulaya imebadilika sana katika muongo mmoja uliopita, lakini kujenga upya mifumo ya ulinzi inachukua muda mrefu zaidi. Urusi inafahamu hilo, wachambuzi wanaonya.
Kwanini Urusi inazidisha vitisho vya nyuklia kwa Magharibi?
Stoltenberg: Ni wakati wa kuruhusu Ukraine kutumia silaha za NATO kwenye eneo la Urusi
Imetafsiriwa na Dinah Gahamanyi na kuhaririwa na Seif Abdalla